Friday 25 March 2016

INAWEZEKANA

Na. Dezidery Kajuna

Kwa kuelewa kichwa cha mada basi ni matumaini yangu kuwa utakuwa umeweza kujua kinachoelezwa katika mada hii. Hata kama imekuwia vigumu kuelewa kichwa cha ujumbe huu basi utakuwa unafahamu fika ni nini maana ya inawezekana. Bidamu wengi tuna imani katika uwezekano wa jambo fulani kutokea. Nachomaanisha hapa ni juu ya uwezekano wa neno, kitu  au jambo fulani kutokea au kufanyika kwa nguvu za kibinadamu au kimungu. Lengo  langu hapa, si kuelezea kile kinachowezekana “kimungu”, hapana nacho nataka kueleza hapa ni juu ya kile ambacho kwa utashi wa kibinadamu kinawezekana.  


Neno “uweza” au “uwezo” bila shaka ni neno lililotokana na neno ”weza”  kwa wataalamu wa lugha ya kiswahili wanaweza kusema, neno weza ni kitenzi kinacho maanisha kustahimili au himili  jambo fulani. Kwa uwepesi kabisa hata maana ya neno lenyewe ni rahisi. Hivyo basi ndugu msomaji, neno uwezo ni ile hali ya kuweza kustahimili au kuhimili jambo fulani.  Ni vivyo hivyo tunaweza pata maana ya kichwa cha mada hii yaani “ inawezekana” 

Mengi yamewezekana hapa duniani kwa sababu tu binadamu ameweza au aliweza kustahimili jambo fulani na hatimaye akafanikiwa.  Wapo wengi sana, tukianza kuwataja  basi ukurasa huu utakuwa ni mdogo sana kunakili majina yote hapa. Kwa mifano mifupi kabisa tunaweza kujifunza kutoka katika historia ya nchi yetu pale mwaka 1950 wakati harakati za kudai uhuru zilipo anza napengine hata kabla ya mwaka huo, na hatimaye iliwezekana na kwa wale walioweza kutuletea uhuru mwaka 1961. Bila shaka sote hatuwezi kumsahau Mwalimu Nyerere pamoja na wenzake. Tukumbuke pia Jinsi Tanzani ilivyokuwa na sauti kubwa katika umoja wa mataifa miaka hiyo ya 1970 mpaka 1985, sauti ile na nguvu ya nchi yetu ilikuwa kubwa kwa sababu viongozi waliokuwepo waliweza kufanya jambo fulani lililoleta sifa hapa Tanzania. Tusisahau pia jinsi tulivyoweza kuwa maarufu kwenye soka, riadha na michezo mingine, kwa kweli ni mafanikio yaliyobaki kwenye historia tu.

Ni rudi kwenye mada yangu, nimelazimika kuanza na mifano ili tuelewe ni jinsi gani mambo yanavyo weza kufanyika na yakatokea.  Tanzania ni nchi ya kipekee sana iliyobarikiwa kuwa na utajiri wa aina nyingi sana. Milima na mabonde ni vichache tu kwa kutaja, mbuga na aridhi bora ni urembo unaotufanya kuheshimika sana, madini, wanyama na misitu vimetufanya tuwe bora kuliko wengine bila kusahau amani tuliyodumisha kila pande ya dunia inatamani kuwa kama sisi. Umasikini tu ndio uliotufedhehesha na kutufanya ile heshima ipotee kwa sababu tu tumeshindwa  kufanya mambo ya maana katika kulijenga taifa letu.  Ni aibu sana kuona kuwa tumeshindwa kuweza kufanya jambo bora kwa maslahi bora ya taifa hili. 

Natambua pia kuwa Tanzania ni nchi pia yenye watu wengi wanaopenda kulalamika bila kuchukua hatua. Malalamiko yamekuwa mengi kuliko uwezo wa kutatua jambo au tatizo  la msingi, nadhani naeleweka hapa. Malumbano yamekuwa wimbo na biashara kwa wengine kiasi kwamba tumesahau wagonjwa walio katika vituo vya afya bila msaada,  tumewasahau wananchi wa kinywa maji machafu bila kupata maji salama, majambazi na vibaka nao wametumia mwanya giza nene kuiba na kupora na kufanya mauaji kwa watu wasio na hatia kwa sababu ya kukosa umeme, ni kwa sababu tu tumeshindwa au hatuwezi kutatua matatizo haya. 

Basi naomba tutoke katika ukanda wa kulalamika na twende kwenye ukanda unaowezekana. Nacho maanisha ni uwezo tulio nao ambao kwa njia moja au nyingine bila shaka tunaweza kubadilika. Inzwezekana kabisa tukawa watu wa kuheshimu uhuru wa mtu na kumuamini mtu pale anaposema anaweza kufanya jambo fulani. Mheshimiwa rahis alipokuwa kwenye kampeni za mwaka 2005 alisema anaweza kuleta maisha bora, tulimwamini na hatimaye tukampa ridhaa ya kutuongoza katika nchi yetu nzuri kwa bahati mbaya ametutawala badala ya kutuongoza kwa sababu maana ya kiongozi ni kusikiliza watu wanasemaje na kisha kutuongoza katika kufanikisha kile tunacho hitaji. 

Tazizo kubwa lililopo ni lawama nyingi kwa Mheshimiwa rais, sidhani kama rais ana makosa, mimi na wewe ndio wenye kosa kwa sababu tulikosa ”uwezo ” wa kutambua kilicho bora na hatimaye tukasema ni bora tu tupate kiongozi. Kwa mara nyingine tulipata nafasi ya kutafakari tena mwaka 2010 hatimaye tukamchagua yuleyule tunaye mlaumu kila siku kwa sababu tu tulikosa ”uwezo” wa kuchanganua na kutambua kwa maono kule tunakokwenda.   Si kosa lake na wala tusimlaumu Mheshimiwa rahis, mwacheni amalize muda aende tutamkumbuka kwa mazuri na kusahu mabaya yake.  Tunaweza kuleta mabadiliko hapa Tanzania ni mim na wewe kufanya maamuzi.

Inawezekana pia, kuwa wengi wetu hatujui kuwa maendeleo ni watu ila ukweli ni  kwamba sisi wenyewe tunaweza kuleta maendeleo mengi na chanya kama unashindwa kuelewa nacho maanisha waulize wachina, watakuambia ni maana ya uzalendo. Uzalendo si tu kuwa mkweli kwa yale unayofanya au kukataa rushwa, uzalendo pia ni kujitoa kwa ajili ya mendelöo ya tafia lako. Tukumbuke uwingi wetu ni tija pia, ila swali ni je tunatumia uwingi huu wa watu kuleta maendeleo? Tunaweza kuleta maendeleo katika mitaa yetu, kwa kujenga mshikamano na ushirikiano. 

Tunaweza changishana pesa tukajenga darasa, tukamlipa mwalimu, tukambadilisha mwenyekiti wa kijiji au mtaa anayefuja pesa yetu na kuleta mwingine. Tunaweza kununua vitabu kwa idadi ya watoto wa kaya zetu. Najua utabisha sana. Ila kumbuka kila jambo linawezekana endapo tutafanya maamuzi yenye tija na yenye kuleta maendeleo. Unasema namaanisha nini hapa? Je umejiuliza ni harusi ngapi mnazochangia kila wiki? Je umejiuliza ni pesa kiasi gani unazotumia katika starehe zinazo zaa ugomvi na jamaa zako? Je haujui kuwa maendeleo ni watu? Je haujawahi kusikia harusi imegharimiwa kiasi cha shilinigi milioni therathini? Au unasema sio wewe uliyechangia pia katika hizo milioni therathini? Kumbuka ”kidogokidogo ujaza kibaba”
Inawezekana kabisa tukawa na barabara nzuri kabisa na  mifereji. Utauliza je huyu mwandishi ana akili nzuri kweli? Ndio nina akili nzuri, Kwani kokoto na changalawe zinatoka ulaya? Nacho maanisha hapa hakina tofauti na kile kinachotokea kule Uchina, si watu waliotumika kuleta maendeleo ambayo yanaifanya china iwe juu kiuchumi leo hii?.  

 Kama hukuwahi kuongea na mchina akueleze kinachotokea kule china. Hata Nyerere alijaribu kuleta wazo hilo, kwani tumesahau wakati alipokuwa akishiriki ujenzi wa reli, barabara, na majengo ya hospitali na shule.  Kule Ghana, rais aliyewahi kuwa madarakani Mheshimiwa JJ Rawlings  alifanikiwa katika hili nalolizungumzia na hata leo wananchi wanatamani arudi madarakani ila katiba hairuhusu.  Inawezekana tukajiletea maendeleo wenyewe kwam misingi ya uzalendo na kujitolea kweli kweli.

Inawezekana, tukahachana na imani za kishirikina tukidhani kwa ushirikina tunataweza kuwa matajiri, wapi bwana! Haiwekani ukawa na mafanikio kwa njia ya ushirikina, hizo ni imani potofu tu. Tumefikia mahali tunaondoa roho za watu kwa sababu tunataka utajiri nani alikuwambia kuwa inawezekana? Tunakata viungo vya albino tukiamani eti tutapata pesa na kisha kuwa matajiri. Kama hayo yangekuwa yanawezekana basi mababu zetu wangetufundisha na bila shaka Tanzania ingekuwa ni nchi ya kwanza kwa utajiri duniani. Kwa maana shirika la habari la uingereza linasema katika utafiti wake kuwa watanzania sawa na asilimia sitini na sita wanaamini katika ushirikina. Je hii ndio sifa bora kuliko zile zilizotangulia, je sifa hi ina ile ya kuwa na sauti katika umoja wa mataifa ipi bora? Vipi kuhusu sifa zile kuwa maarufu kwenye soka na riadha kipi bora tukilinganisha na ushirikina huu?

Inazekana tukabadilika kimawazo na kimatendo, tukumbuke kuwa hata viongozi tuliokuwa nao ambao siku zote wametufanya kuwa wajinga tunaweza kuwabadilisha muda wowote. Inawezekana tukagoma kushirikiana na kumtambua kiongozi wa aina yoyote ile kama haturidhishwi nae kitabia, kimaamuzi, na kiuwezo katika uongozi. Ni wewe na mimi kufanya maauzi kwa sababu inawezekana. Sitangazi mapinduzi ila naeleza uwezekano ulio katika mikono yetu au ndani yetu.
Inawezekana tukakomesha rushwa maana nayetoa rushwa ni mimi na wewe. Nani asiyejua kuwa rushwa ni adui wa haki? Lakini sote tumeamua kuabudu rushwa. Mfano mzuri ni kipindi kile nikiwa mwanafunzi pale chuo kikuu cha Dar es Salaam nilipokuwa naenda kwenye mahakama zetu hizi, ukifika pale masijara wanataka pesa ili uweze kusainiwa karatasi kwa mhuri wa hakimu. 

Wapi kwenye katiba ilipoandikwa kuwa mahakama lazima zitoze fedha kwa wanafunzi wanaoenda kuomba msaada huo wa kisheria mahala pale? Bila shaka hakuna, kwa wanasheria watanisaidia kwa hili. Nacho fahamu ni kuwa kama nikienda kwa mwanasheria wa kujitegemea anaweza omba pesa au la maana ni haki  yake, na kwa sababu analipia mhuri ule kila mwaka ni haki yake kufanya hivyo ila si haki ya mahakama. Inawezekana kabisa tukarikemea jambo hili na kulitokomeza kabisa pamoja na rushwa zingine zote.

Inawezekana pia tukawa na shule zenye majengo bora na vyoo bora. Nani asiyejua kuwa kuanzia mijini mpaka vjijini shule hazina vyoo? Je ni kweli wanachi tumeshindwa kujenga vyoo?, hata kuchimba shimo tu?, Inawezekana kabisa tukaleta maendeleo sisi wenyewe. Kama tunaweza kuchimba makaburi tunashindwaje kuchimba vyoo? Au ni raha sana kuona wanafunzi wadogo na wahalimu wakiingia vichakani kujisadia na Je mtoto wako akibakwa au kung’atwa na nyoka huko vichakani utamlaumu nani? Tubadilike, turudi katika enzi za kujitolea na kujitegemea kwa maana nina imani kuwa tunaweza. 

Inawezekana tukabadilisha mitaala ya elimu yetu ikawa mingine na yenye uwezo wa kuzalisha wanafunzi walio bora na wanaoweza kujiajiri wao binafsi bila kutangatanga katika mitaa ya posta kutafuta ajira bila mafanikio. Upungufu wa ajira umezaa rushwa, tena ruswa zingine ni za ngono. Inauma sana ila je alaumiwe nani kwa hili?  Inawezekana kabisa kutokomeza rushwa za namna hii ila tumeshindwa kufanya maamuzi hayo tungali na uwezo huo.

Inawezekana kabisa, wanafunzi wanaomaliza elimu ya vyuo vikuu wakakopeshwa pesa kutoka katika benki mbalimbali hapa nchini na hatimaye wakajiajiri. Lakini je wamepewa elimu ya kujiali? Je serikali inawasaidia kisheria kupata mikopo bila rushwa au  riba kubwa? Nani wakuwatetea kama sio mim ina wewe? Inawezekana mim ina wewe tukaleta maendeleo, tukubaliane katika hili. Kama tatizo ni uongozi basi tujiulize kabla ya maamuzi, ni nani anaweza kutuletea mabadiliko ya kweli?

Inawezekana kabisa tukaishi katika jamii yenye amani bila kubaguana kwa misingi ya dini au kabila. Tumeacha watu wachache wanachezee amani na mshikamano wetu kwa kutubagua kwa misingi ya dini na ukabila. Hili la dini ndilo swala muhimu na nasisitiza kuwa inawezekana kabisa tukaishi katika jamii ambao hatutatambuana kwa misingi ya dini au kabila bali kwa misingi ya michango katika kuleta maendeleo. Tutamjua mvivu asiyefanya kazi, asiyepeda ushirikiano, mla au mtoa rushwa, mwizi au jambazi na makundi mengine yasiyo faa katika jamii yetu na si nani ni muislamu au mwikristo.

Japo yapo mengi yanayowezekana tatizo ni maamuzi, hatujafanya maamuzi na sijui tunangoja nini. Tubadilike, kama wewe ni kijana badilika na tambua kuwa inawezekana ukawa na maisha bora bila kutemea mtu mwingine, wazazi pia wanaweza kuleta maendeleo kwa kusisitiza kujituma, kufanya kazi kwa bidii, kupunguza lawama, kujitoa katika shughuli za maendelo na hata kuubadilisha uongozi usiofaa. Tubadilike, tufikirie, tufanye maamuzi yaliyo na tija kwa maendeleo ya taifa letu.


No comments:

Post a Comment