HESHIMA HAINA UMRI!
Na. Dezidery Kajuna.
Ni asubuhi ya saa tano, natoka ndani ya nyumba ninayoishi katika mtaa huu
wa Prästgatan hapa nchin Swedeni tayari kwa ajili ya kwenda shule maarufu kwa
jina la SFI (Svenskundervisning
för invandrare) kwa lugha ya kiswahili ikiwa na maana
ya elimu ya lugha ya kiswidi kwa wahamihaji au wageni. Ni shule mahususi kabisa
kwa ajili ya wale wanao penda kujifunza lugha hii ya kiswidi ili iwe rahisi
kwao kuwasiliana na wenyeji.
Sababu kubwa ya wageni kujifunza lugha hii ni muhimu kwani lugha
itumikayo katika nchi hii ni kiswidi kila utakapokwenda hapa nchini Sweden. Ni
tofauti na nchi nyingine kama Uingereza, Marekani na Australia ambako lugha
muhimu ni kiingereza. Tofauti kabisa na
Sweden, Norway, Finland, Ujerumani, Denmark na nchi nyingine ambako lazima
usome lugha yao kwa mawasiliano ya kawaida katika jamii zao. Jambo zuri ni kuwa
katika nchi hizi ofisi zote za serikali pamoja na vyuo vyote vinatumia lugha ya
kiingereza kwa ajili ya wageni na lugha yao kwa ajili ya wenyeji.
Hali ni tofauti kabisa hapa nchini Sweden kwani lugha kama ilivyo mahala
pengine ni muhimu kwa mawasiliano. Serikali ya Sweden kupita halmashauri zake
zinatoa fursa ya bure kwa watu wote, haijalishi wewe ni mkimbizi, mhamiaji
haramu au ni mgeni wa kawaida kama vile mwanafunzi au mtalii kujifunza lugha ya
kiswidi
Makundi hayo yote yana haki ya kupata fursa ya kusoma kiswidi bure bila
kutoa senti mfukoni mwako. Cha muhimu ni kuwa na namba ya uraia, hili ni jambo
geni sana Tanzania, na sidhani hata kwa
miaka ishirini ijayo kama tunaweza kufikia hatua hii ambayo wenzetu wa Kenya
labda wanaweza kuwa wamefikia.
Ukungu ni mwingi barafu likiwa limepukutika sana na nimevaa viatu si kama
hivyo navyotumia nikiwa natoka kwa mama Mtey (mwenye nyumba) hapo ubungo kwenda
mjini hasa posta ya zamani kutafuta kazi katika maofisi.
Kipindi cha baridi na haswa kipindi cha barafu inakulazimu kuvaa viatu
maalumu kwa ajili ya kuweza kutembea salama katika barafu ili usianguke na wala
miguu isiweze kuganda kutokana barafu.
Wakati huo huo umevaa makoti mazito kwani baridi hili si mchezo kama
haukupata mlo wa kutosha lazima tumbo lilalamike. Katika mtaa huu kila
unayekutana nae anahema huku akitoa moshi mdomomi si kwamba wanavuta sigara la
hasha! Ndilo baridi lilivyo mwili unakuwa umepigwa baridi kiasi cha kufanya
mvuke utoke ndani ya kinywa.
Najikongoja taratibu, navuka barabara huku ni kibonyeza kitufe chekundu
ili taa za barabarani ziweze kisimamisha magari nami nipite niende zangu
shuleni. Nakatiza uwanja bila shaka nimefika shuleni, wanafunzi wachache wapo
nje wanavuta sigara maana huku ni kawaida sana kutokana na hali ya hewa.
Nalazimika kusafisha viatu vyangu kwanza ili niingie ndani maana barafu
limeganda kwenye viatu vyangu mithili ya matope ya soko la Tandale. Naingia
ndani ya jengo la shule kabla sijaingia darasani napita sehemu yenye komputa
nyingi mahsusi kwa jaili ya wanafunzi ghafla nasikia mtu anaita Eric! Eric!
Eric!
Kisha nageuka, kuangalia nyuma naona mtu wa makamo sana akiwa amesimama
karibu na komputa akiwa na begi kubwa mithili ya msafiri nami namsogelea
nisikilize anasemaje.
Kumbe wakati anaita Eric! Alikuwa ananiita, nilimwitikia kwasababu Eric
ni rafiki yangu wa karibu na ni mwanafunzi mwenzangu kutoka Ghana bila shaka
nilijua mzee huyu amenifananisha na rafiki yangu. Kama utamaduni wangu
nikamsogelea, tukasalimia na mara hii anaonyesha heshima sana kwangu japo
haukuwa utamaduni wake kumbe anashida, jana yake alikuwa amelala nje kwa maana
shirila la nyumba lilimfukuza na baridi hii nilimwonea huruma sana.
Cha msingi nilitaka kusikiliza anasemaje. Ananiuliza kama naweza kumsitiri
au kama namjua mtu yeyote mwenye chumba cha ziada maana mtu aliyekuwa anaishi
nae na ambaye ndie aliyekuwa mpangaji halali amefariki na hivyo kisheria hapa
nchini Sweden lazima uondoke maana kimkataba hautambuliwi. Jawabu nililo mpa ni
kwamba sina sehemu ya kumsitiri kwa muda ule maana na mimi naishi mtu na kwa
wakati huo sikuwa na taarifa juu ya mtu mwenye chumba cha ziada.
Kwa msaada tu nampa majina ya kampuni mbali mbali zinazohusiana na vyumba
vya kupanga. Kisha namtakia kila lakheri, naondoka zangu nikimuacha na
masikitiko maana labda alidhani ndo tatizo limeisha, ukweli maisha hapa ni
magumu hasa ukiwa huna mahala pa kuishi, kwa kweli ni kazi.
Kipindi hiki cha baridi kali kimekuwa hatari huku ulaya. Ulaya Mashariki, watu wengi zaidi ya mia nne
wamepoteza maisha wengi wao wakiwa wazee na wale wasio kuwa na makazi maalumu.
Baridi hili kama hauna kipoozeo (heater) basi ujue unakufa maana barafu hili
likiambatana na baridi mara nyingi upelekea damu kuganda na hivyo upelekea
maumivu katika sehemu mbali mbali nyingi za mwili hasa kwenye vidole na kwenye
paji la uso.
Mzee huyu kwa jinsi nilivyomuona basi atakuwa amepata taabu kweli katika
usiku uliopita. Mzee huyu si mzungu jamani! Ni mtu mweusi kama mimi, yeye
anatoka Kameruni, nchi yenye mchezaji soka maarufu wa kimataifa Samuel Eto’o!
Aliwahi kufika Tanzania na wasakata kambumbu wenzake.
Huku, Sweden, kila katika mji utakaoenda hautakosa mkameruni, maana ni
wengi sana mithili ya wachagga ambao wametapakaa kila mkoa Tanzania wakifanya biashara. Ila wakameruni
hawa hawafanyi biashara, wao wapo huku kwasababu za kimaisha. Kameruni maisha
ni magumu sana na hivyo wengi wanazamia huku na sehemu zingine za Ulaya. Uzuri wakameruni ni uwezo wao katika lugha,
wanaweza kuzungumza lugha ya kiingereza na kifaransa kwa ufasaha sana. Na ni wa
watu wanaojituma sana katika kufanya kazi.
Si kwa mazuri hayo tu bali nao wanaubaya wao, kwa mtazamo wangu ni watu
ambao wanaubaguzi sana, wabinafsi, lakini cha kushangaza sana ni kwamba
wanadharau sana watu kutoka Afrika ya Mashariki. Maana wanaona uchache wetu
hapa nchini Sweden ina sehemu zingine za Ulaya basi wanadhani sisi si watu
wakujituma, ni waoga, na hatujui lugha.
Tuendelee na mzee wetu, basi mzee huyu ni mmoja kati wa ya watu
wanaodharau sana vijana, hasa wa kiume. Mara
nyingi huongea vizuri na vijana wa kike hasa wanaotoka bara la Afrika. Hata
wakameruni wenzake huwadharau pia ndio maana hakuweza kupata msaada kutoka kwa
wakameruni hao kwa maana wanamfahamu sana.
Bila shaka walimtenga kwa sababu ya dharau zake!
Kwa sababu ni wa makamo basi alidhani yeye ni bora kuliko wadogo la
hasha! Hiyo si sababu kwa maana inawezekana kijana mdogo akawa na hekima kuliko
mtu mzima nikakumbuka msemo wa Kiswahili;
”mtu mzima hovyo”!
Si watu wote wazima
wanahekima wengine ni hovyo kweli kweli! Cha msingi nachodhani ni muhimu ni
heshima, mdogo aheshimu mkubwa na kubwa afanye vivyo hivyo kwa wadogo hapo
maisha yakutakuwa na amani vinginevyo vijana watacharuka. Hawana simile vijana
wa siku hizi ati.
Heshima ni alama ya upendo pia, maana kama hauna
heshima kwa mtu mwingine maana upendo kwa mtu yule imepotea .
Ni muhimu kujenga heshima kama kweli tunapenda upendo uwe kati yetu.
Jamii ya Tanzania kwa sasa inatazamwa kama jamii yenye maadili yaliyoporomoka
sana kupita kiasi. Vijana wadogo wanatukana wazazi wao, wanabaka walimu,
wengine wamepotelea katika matumizi ya
madawa ya kulevya, vitendo wizi na ujambazi na wengine kwenye biashara ya
ngono.
Heshima ni jambo la muhimu sana, kwani haijalishi wewe ni nani na umri
gani. Kwa sisi waafrika utamaduni wetu unatufunza kuwa watu wenye heshima mara
zote kwa watu wazima na wadogo. Tunahitaji kuwasaidia walimu kuanzia shule za
awali, msingi, sekondari mpaka vyuo kuimarisha na kusisitiza heshima, upendo na
kujitoa kwa ajili ya manufaa ya jamii. Hivi vyote vikipotea basi hata uzalendo
hautakuwepo kamwe!
Tusibaki kuwa watu wa kulalamikia rushwa, uongozi uliodorora na maendeleo
duni. Hivyo vyote uanzia nyumbani kwa wazazi na watoto. Lazima kaya zetu zijengwe
na upendo, uzalendo na heshima ili taifa liwe na watu wa aina hiyo. Bila shaka
wale walio viongozi bora leo hii hapa Tanzania na sehemu nyingine duniani wana
historia nzuri toka huko walikotoka wangali watoto na hatimaye baba au mama wa
familia. Tubadilike na heshima tusisitize kwa rika zote!
No comments:
Post a Comment